KISWAHILI 2-MADA 1 : FASIHI KWA UJUMLA NADHARIA YA FASIHI-



MADA 1  : FASIHI KWA UJUMLA
NADHARIA YA FASIHI
Nadharia niImani au kanuni zinazofuatwa na watu Fulani au jamii katika shughuli au jambo Fulani mahsusi.
Nadharia za fasihi ni muongozo au kanuni zinazofuatwa na wataalamu (wanazuoni) mbalimbali wanapoteua maana halisi ya fasihi.
Fasihi ni nini?
Fasili/Maana mbalimbali zimetolewa kuhusu dhana ya fasihi, maana hizo ni kama:-
1.      FASIHI NI KIOO CHA JAMII (MAISHA)
Kwa maana kwamba mtu anaweza akajitazama akaona taswira yake na akajirekebisha . Fasihi hii ina udhaifu kwani kioo hakiwezi kumweleza  mtu jambo la kufanya ili hali yake iwe bora zaidi . Pia si sehemu zote takazojiona kwenye kioo(F.Mkwera , 1978)
2.       FASIHI NI HISI
Fasihi ina maana kuwa lazima pawe na mguso fulani wa wahusika ndipo aweze kuandika na kueleza jambo fulani,’Sengo na kiango  Wanasema “hisi ni kama kuona njaa, baridi, joto, uchovu pengine kuumwa. Hapa swali la kujiuliza ni kwamba, je fasihi ina maana moja kati ya hiyo? Uamuzi wa kutenda jambo huja wakati umeguswa. Je hizo hisia ziko wapi? Je mtu ambaye haguswi  sana moyoni hawezi kuwa mwanafasihi  mashuhuri? Je mwanamuziki ambaye huusifu uzuri wa mwanamke anaguswa moyoni? Je mwandishi kama Shaban Robert,  E. Kazilahabi wameguswa mara ngapi? Vile vile kivipi waguswe Zaidi ya wengine?  (Sengo na Kiango) hivyo bado fasili hii ina madhaifu
3.        FASIHI NI MWAMVULI WA MTU NA JAMII NA UTU NA MAISHA YA HADHI NA TAADHIMA.
Fasihi  hii ina maana kwamba mwamvuli humkinga mtu katika mvua na jua na fasihi huhifadhi na kukinga amali za jamii zisiharibike maana hii ni nzuri kwani inasisitiza utunzaji wa kile kizuri kwa maana kuwa jamii inachambua kuwa makini na kuona amali za jamii zinazihifadhiwa. Lakini swali la kujiuliza ni  kwamba jamii itasaidiwa?
Jamii haitulii kama maji katika mtungi  bali hubadilika mara kwa mara kutokana na nguvu za migongano, hivyo kitu kipya huzaliwa na cha zamani hufa kwasababu jamii haitulii, hivyo hakuna haja ya kuhifadhi amali za jamii chini ya mwamvuli. Zipo mila na desturi zilizohifadhiwa na makabila mengi ambazo hazina nafasi leo. Hali ya mabadiliko ya jamii kutokana na siasa, utawala, uchumi, elimu, sayansi na teknolojia vyote hivi katika maendeleo vitatoboa mwamvuli na kuziharibu amali zilizohifadhiwa (Sengo na Kiango 1973)
4.       FASIHI NI SANAA YA UCHAMBUZI WA LUGHA YOYOTE KADRI INAVYOSEMWA,INAVYOANDIKWA NA KUSOMWA
Hii ni kweli kuwa fasihi lazima itumie lugha kwani lugha ndicho chombo muhimu kitumiwacho na fasihi na si fasihi  tu bali taaluma zote hutumia lugha.Madhaifu/Udhaifu wa fasihi hii ni kwamba maana hii imejikita katika uchambuzi wa Lugha kana kwamba hakuna vipengele vingine vinavyochambuliwa katika fasihi zaidi ya lugha na hii ni sawa na kusema umeme ni waya wa shaba kwa vile umeme umepita kwenye waya huo.Na hii ni si kweli kwani Hisabati,fizikia au historia si fasihi kwa vile tu hutumia lugha.
V:FASIHI NI KIELELEZO CHA HISIA ZA MWANDISHI JUU YA MAMBO YANAYOMWATHIRI YEYE,KIKUNDI AU JAMII NZIMA ANAMWISHI NA KWAMBA LENGO LAKE NI KUSTAREHESHA AU KUFUNZA WASOMAJI.
Fasihi(maana) hii ni nzuri kwa ujumla lakini mapungufu yake ni kwamba imemuwekea mwandishi kama chanzo pekee cha uumbaji wa Sanaa na hasa akili yake pia maana hii imetokana  na falsafa ya kidhaanifu kwa kuhusisha uchambuzi wa mambo katika fikra bila  kutazama hali halisi ya maisha ya watu na vitu.
VI:FASIHI NI CHOMBO CHA UTETEZI WA MASLAHI YA TABAKA MOJA AU JINGINE NA KWAMBA MWANDISHI NI MTUMISHI WAKE AJIJUAYE AU ASIYEJIJUA ATAKE ASITAKE MWANDISHI HUYU NA LENGO AU DHAMIRA FULANI ANAYOTAKA KUIONESHA.
Wasomaji wanaweza wakipenda au kuyataka maudhui ya kazi yake na pengine jamii kufuatana na msimamo juu ya itikadi ya siasa (nap engine amali za jamii)inayotawala kwa kipindi kile  na jinsi mwandishi anavyoanisha maandishi yake na itikadi hiyo.
Fasihi au maana hii ni nzuri sana kwani kwa kifupi ni kwamba fasihi ni silaha nyingi zinazotumiwa na tabaka moja kutetea maslahi yake katika mapambano ya kudumu dhidi ya matabaka mengine.
Hitimisho kwa ufupi fasihi ni taaluma inayotumia Sanaa maalumu ya lugha.Taaluma hii ni elimu ambayo ndiyo maisha yanayofaa kufuatwa na jamii katika maendeleo yake kisiasa,kiuchumi na kiutamaduni.Ni elimu kwa sababu fasihi huipa jamii maarifa na mbinu za kupambana na mazingira na kuondoa uozo katika jamii kwa ujumla.
Fasihi hutuelezea uzuri wa maandishi ,maandishi ambayo huonekana katika mashairi historia za maisha ya watu,tenzi,hadithi za kusisimua na insha mbalimbali.
CHIMBUKO LA FASIHI NA SANAA.
Kuna mitizamo mikuu miwili ya kiulimwengu inavyotokeza katika suala la chimbuko la fasihi .Mitazamo hiyo ni ule wa kidhanifu na ule wa kiyakinifu.
I.MTAZAMO WA KIDHANIFU.
Mtazamo wa kidhanifu wa misingi yake katika kudhanifu kwa hiyo hufuatana na mtazamo huu inaaminika kuwa fasihi na Sanaa kwa ujumla kutoka kwa Mungu kwa hiyo mwanasanaa ikiwa imekwishwapikwa na kuivishwa na Mungu huyo.
Mtazamo wa namna hii ulijitokeza tangu zamani sana wakati wanafalsafa wa mwanzo wa kigiriki na kinenzi kama vile Socrafes Plato na Anstolle,walipoanza kuingia katika ulimwengu wa nadharia ya Sanaa katika uwanja wa nadharia wa fasihi/Sanaa ya Kiswahili kuna mifano mingi ya wahakiki wa mwanzo waliokuwa na mitazamo sawa nay a wanafalsafa hao mfano F.Mkwera  insha yake fasihi inadhihirisha uaminifu wake wa mawazo ya kidhanifu kwa kudai “fasihi ni Sanaa ambayo huanzia kwa muumba humfikia mtu katika vipengele mbalimbali ni hekima ambayo mtu ameshirikishwa apa kumtambua muumba  wake”.
Nkwera ameungwa mkono na wahakiki wengine ambao wanasisitiza mtazamo huu kwa kusema
                “Mtengenezi ya Sanaa huonekana kuwa ni shughuli ya kiungu yenyekumwiga Mungu ambaye ndiye msanii wa kwanza”
John Ramadhani pia katika makala yake ya fasihi ya Kiswahili anasisitiza kuwa.
Zaidi ya kwamba fasihi ni hisia vile vile kitengo cha mtu cha kubaini kazi ya Sanaa ni uigaji wa Mungu ambaye ndiye mfalme wa Sanaa zote”.
Mawazo haya ya akina Nkwera,John Ramadhani na wengineo wa aina hiyo mwangivi tu mawazo yaiyochakaa ambayo yalikwisha kutajwa na kushughulikiwa  na wahakiki wa zamani tuliowataja kwa msimamo huu wa kidhanifu,Sanaa au fasihi havijifinyangi kwa jitihada zab akili za mikono ambayo mtu hana uwezo wa kuiona.
Mtazamo huu Zaidi ya kuwa umepotosha maana halisi kwa kuchanganya Imani na taaluma,pia unajaribu kumtenganisha msanii na jamii yake unatoa nadharia inayomwinua msanii na kufanya aonekane kuwa  mtu wa ajabu aliyekaribu na Mungu kuliko watu wengine wa kawaida.
Athari za mtazamo huu zinaonekana hata leo hii kwa baadhi ya wataalamu wa fasihi ya Kiswahili waliojaribu lueleza maana ya ushairi wengi wao walidai kuwa ushairi ni hekima za ajabu pamoja na mawazo ambayo yana uzito na kustajabisha kwa hiyo hata washairi wenyewe ni lazima basi wawe na hekima na mawazo hayo mazito ambayo aghalabu tunayaona wakiyapokea mara kwa mara  kutoka kwa Mungu katika beti zao za mwanzo za mashairi au tenzi zao.Pia tunawaona wacha Mungu hawa wakimshukuru Mungu wao kwa kuwapa vipaji hivyo ambavyo kuwanyima wengine katika beti za mwisho za mashairi yao.
MTAZAMO WA KIYAKINIFU
Chanzo cha fasihi kulingana na mtazamo huu si sawa na chanzo cha binadamu wenyewe.Binadamu na mazingira yake ndio Alfa na Omega ya fasihi.
Iwe kwa kuumbwa au mabadiliko kuanzia chembe hai ambayo imepitia maendeleo kadha ya mateuzi hata kufikiria mtu binadamu alionishwa na kazi ili kuyabadili mazingira yake.
Katika harakati zake za kujiendeleza kiuchumi kila mara alijaribu hiki na kile alichokiona kinafaa alikiendeleza Zaidi na kukidumisha katika hali hii hadithi(ngano),methali,vitendawili,nyimbo,tenzi(mashairi) n.k vyote hivyo vilitungwa na kusimuliwa kwa madhumuni  ya kufunza,kukosoa,kuadhibu,kuchokoza fikra na kuliwaza jamii baada ya kazi.
Sanaa hii ilirithishwa toka kizazi hadi kizazi kwa njia ya masimulizi na binadamu ilivyozidi kujiendeleza kisayansi na kiteknolojia akahifadhi taaluma hii katika maandishi.Ndiyo sababu tunasema chanzo cha fasihi ni sawa na chanzo cha binadamu mwenyewe na jinsi binadamu alivyozidi na atakavyozidi ndiyo taaluma hii ilivyokuwa na kuendelea.

DHIMA YA MWANAFASIHI KATIKA JAMII
Maana ya mwanafasihi/mtunzi wa kazi ya fasihi
Ni mtu yeyote anayejishughulisha na uandishi au utungaji wa kazi za fasihi yaani fasihi andishi na fasihi simulizi.
DHIMA ZA MWANAFASIHI
1.(a).Kuelimisha jamii,Katika kuelimisha jamii mwanafasihi huchambua na kuchochea umma kuwafumbua macho,hufichua wazo au uchafu uliomo katika jamii,wagandamizaji kufichuliwa na wagandamizao hupewa muongozo sahihi ili waitambue hali yao dhaifu.Mfano”Duka la Kaya”kuchambua na huchochea jamii ili iweze kupambana na hali mbaya ya maisha.
(b).Kupiga vita kwa hali na mali mazingira yote ya ujinga,maradhi,njaa na umaskini,Mfano mwandishi wa tamthiliya ya Hawala ya fedha anapambana na maovu kama vile ujinga na uvivu na Ngoswe Penzi Kitovu cha Uzembe anajali na kupiga vita.

(c).Kukosoa jamii,Mwanafasihi anaikosoa jamii katika vipengele mbalimbali vya maisha.Mfano riwaya ya “Duka la Kaya”inakosoa hali ugawaji mbaya wa bidhaa muhimu nchini “Raha karaha na Mashairi ya Chekacheka”mwandishi wa diwani hizi anaikosoa jamii ya Tanzania kwa mapana kama vile Uongozi mbaya,kukithiri kwa rushwa n.k.
(d).Kutia hamasa na kumfanya mtu asikate tamaa,Mfano S.Kandoro anaeleza hamasa ya wananchi waliokuwa wameungana kama “Siafu ili kumtoa nyoka pangoni”.Mwandishi kwa hamasa amewaita waafrika njooni “au” kwetu ni kwa nini.Hivyo ni wazi kuwa kazi hizo zinajitahidi kuendeleza mapambano dhidi ya ukoloni mkongwe na mambo leo.
(e)Mwandisi anadhima kujenga misingi na fikra za usawa na demokrasia miongoni mwa umma wa wakulima na wafanyakazi,Mwanafasihi huyu huwatukuza wakulima na wafanyakazi pamoja na amali zao.
(f) Mwanafasihi hueneza mawazo na falsafa za jamii,Kwa mfano katika shairi na ngonjera za Mathias Mnyapala ametangaza sana siasa ya ujamaa na kujitegemea kwa kutumia ngonjera za UKUTA 1 & 2 vile vile riwaya kama vile mfaa na utu,njozi za usiku,ndoto yandaria ,jero si kitu n.k zimetangaza sana siasa ya ujamaa na kujitegemea hapa nchini Shaban Robert aliwahi kueneza falsafa juu ya kweli kwa kiasi kikubwa katika mashairi yake.
(g)Mwanafasihi hutoa mwongozo kwa kuikomboa jamii kutoka fikra mbovu za kugandamizwa,kunyonywa na kuonewa na kujikomboa ili iweze kupata haki na usawa,Mfano Riwaya ya kiimbila “Ubeberu Utashindwa” na tamthiliya ya E.Mbogo “Tone la Mwisho” G Husseni “Kinjekitile”
2.Kuburudisha,zipo kazi mbalimbali za fasihi zinazoburudisha.Msomaji au msikilizaji wa fasihi huburudisha yaani husisimsha mwili na akili na huvutiwa kihisia na kazi ya fasihi anayeisoma au kusikiliza.Tabia ya msomaji au msikilizaji huweza kujengwa kutokana na mafunzo na mifano bora ya matendo ya kuigwa anayoyapata katika fasihi.
3.Kuhifadhi na kurithisha amali za jamii,Amali za jamii ni pamoja na mila na desturimtindo wa maisha,Imani historia jiografia,visasili na visakale ni urithi ya maarifa ya kijadi kwa mfano tiba sayansi ya kilimo,mbinu za uwindaji,ufundi wa aina zote n.k.Amali hizo huweza kuhifadhiwa na kuendelezwa na mwanafasihi na hivyo kurithishwa kwa vizazi vijavyo.
Kwa mfano tamthiliya ya Kinjikitile inahifadhi mengi kuhusu hali ya maisha wakati wa ukoloni wa kidachi,Kurwa na Doto (farsy) ni riwaya yenye kuhifadhi japo kwa kejeri,mila,desturi na itikadi za jadi za waunguja,Riwaya ya Bwana Mnyombokero na Bibi Bugonoka Ntuhanalwa na Buliwali iliyoandikwa na Anicet Kitireza imehifadhi mila,Imani,mtindo wa maisha,ufundi na taaluma mbalimbali za jadi za wakerewe mengi yaliyoeleza humo siku hizi hayapatikani popote isipokuwa katika riwaya hiyo vile vile Mzishi wa Baba ana Radhi(Nkwera) kinaeleza mila na desturi za wapangwa.
Watunzi hasa nyimbo na visasili hukoleza pia shughuli za kijadi za kiutamaduni kwa mfano Ibada,matambiko,sherehe,katika shughuli za aina hiyo nyimbo licha ya kuwa kiburudisho hubeba ujumbe wenye kuhusiana na tukio hilo.
4.Kudumisha na kuendeleza lugha,Kwa kadri lugha inavyotumiwa na kufinyangwa na watunzi ndivyo inavyokuwa na kupevuka.Maneno mengi yatumiwayo leo katika lugha mbalimbali yalibuniwa na kuenezwa na watunzi wa mashairi,riwaya,nyimbo na tamthiliya katika Kiswahili.Mifano mizuri ni maneno mengi yahusuyo Sanaa ya ushairi(vina, mizani, beti, mishororo, miwala, tathlitha, takhimisa, tarbia n.k)
Katika adi ya ushairi wa kiswahili inadaiwa kuwa ushairi ulikua ni ghala ya maneno washairi walitumia maneno magumu au yasiyokuwa ya kawaida makusudi ili kuyahifadhi ysipotee…….katika tamduni nyingine kazi hiyo hufanywa na kamusi na vitabu viitwavyo Hazina ya maneno kwa kuwa waswahili hawakuwa na kamusi kazi ya kuhifadhi maneno ilifanywa na ushairi.
FASIHI NA JAMII
Fasihi ni zao la jamii. Ni zao ambalo ni chombo vilevile chs jamii hiyo ambayo kinaweza kutumiwa kwa shari au kwa heri. Inaweza kutumiwa kusaidia kuchonga wanajamii ili wayaangalie mazingira yao kwa udadisi na uchambuzi ili wayarekebishe. Vile vile inaweza kutumia na tabaka fulani kuwapumbaza au kuwatia kiwi machoni wanajamii wasiweze kuyaangalia kwa jicho pevu mazingira hayo. Hivyo wakashindwa kuyaelewa vizuri na hivyo wasifanikiwe kuyapindua machungu yanayowasakama.
Hivyo fasihi yapaswa kuwa chombo cha uaminifu kwa jamii yake. Fasihi ya kweli kwa jamiihaina budi kuichambua, kuikosoa, kuielimisha na kuiongoza jamii, kuondoa unyonge na upotofu wa aina yoyote ambao upo katika jamii.
Vile vile fasihi inawajibika kuonyesha bila kuogopa udhalimu wowote uliomo katika jamii na ambao unaendelea kujiimarisha na kutabiri hali mbaya ya jamiihiyo pia lazima ionyeshe mambo yote mazuri katika jamiina kuyasisitiza na kuwatia moyo wale wanayotenda ili waendelee kuyatenda na kueneza uzuri huo kwa wanajamii wote.Fasihi haina budi kupinga aina yoyote ya upotofu na kufichwa makosa yake katika jamii. Pia inapaswa kushambulia udhaifu wowote uliomokatika jamii.
Fasihi ni mali ya jamii hivyo inapaswa kuwa mali ya jamii kweli iweze kuleta maendeleo ambayo jamii hiyo imepanga kuyaleta. Vile vile watu wanaokwenda kinyume na utaratibu wa jamii fasihi haina budi kuwataja wazi wazi na kuwakemea bila kuogopa ili waweze kujirekebisha na kushirikiana na  wazao katika kuzungusha gurudumu la maendeleo ya jamii.
Ili fasihi iwe chombo kiaminifu cha jamii hiyo lazima  ionye, ikosee, na kurekebisha jamii wale wanaotenda mambo kinyume na falsafa ya jamii hiyo lazima wakosolewe. Fasihi iwaseme wazi wazi wale wanaotenda kinyume cha matakwa ya jamii hiyo lazima wakosolewe. Iwakosoe wale wanaofanya mambo yasiokubalika katika jamii na inapobidi kulaanina kukemea matendo yote yasiyofuata mwenendo wa jamii inayohusika.
Msimamo wa mwandishi ndio utakaofanya fasihi yake ambayo kwa kweli ni fasihi ya jamii. Iwe chombo kiaminifu katika kuyapindua machungu , makosa hayo kimsingi kuna misimamo miwili kuhusu fasihi na jamii.Plekhenou (1957)anaitaja misimamo hiyo:-
i)                    Wapo wanaoamini kuwa Sanaa ni chombo kimoja wapokatika harakati dhidi ya mazingira, msimamo huu unasisitiza kuwa Sanaa isaidiwe kumsukasuka na kumwamsha mwanadamu ili apambane na mazingira machafu. Msimamo huu unasisitiza kuwa jamii hapo kwa aili ya mwanasanaa. Mwanasanaa yupo kwa ajili ya jamii.
ii)                   Wapo wanasanaa wanaosisitiza kuwa kufanya Sanaa kama chombo tu ni kuzalilisha mno. Sanaa si lengo si chombo Plekhenou  anasema kwa kuwa watu hawa hudai kuwa kuifanya sanaa chombo cha kufikia malengo hilo ni maalumu mno ni kuteremsha hadhi ya Sanaa. Ili fasihi iwe na manufaa katika jamii ni hima iwe chombo kiaminifu cha jamii hiyo, eti lazima iwe na jukumu la kuielezea, kuichambua, kuikosoa, kuiongoza jamii katika lengo lake la kuipindua unyonge na uchafu uliomokatika jamii. Iwe na msimamousiotetereka, usimhofu mtu, usiogope kitu, itetee haki, ipinge na kufichua makosa yafanyikayo katika jamii, ioneshe udhaifu wa aina zote katika jamii. 
Somoro (1977) katika kusisitiza hayo yeye alisema “Ni lazima kufahamu kuwa, ujinga wa mtu mmoja ni udhaifu wa jamii nzima na uathiri kazi ya kila mmoja wetu……makosa ya mtu mmoja huifanya kazi ya kila mtu kuwa nzitozaidi kuhatarisha malengo yetu na kuidhoofisha jamii nzima. Waandishi wasione haya kuyataja makosa yanayofanyika katika jami wanakosolewa nao wasione haya wala chuki bali wafurahi kuwa adui amegunduliwa.
Lunacharsky (1973)baada ya kukosolewa Sanaa na kuimarika kutokana na kukosolewa huko alisema:-
“Hata kama tumezorotesha mambo kiasi kikubwa na wakati mwingine kufanya makosa mazito, kizazi chetu kinajivunia kwa mazito mengi tuliyoyafanya na tuko tayari kukubali hukumu za vizazi vipya bila hofu….,”
Anasisitiza Lunacharsky hapani muhimu fasihi ipongeze watu kuwa michango wanayofanya katika jamii, lakini isiogope kuwa hukumu wanaopotosha jamii. Ni muhimu fasihi ieleweshe umma itusaidie umma kutambua kuwa pengine maarifa yetu ya jana ni ujinga wa leo.
Katika kusisitiza hiloAblilatif Abdallah anaeleza kuwa fasihi sharti izingatie na kushughulikia matatizo ya jamii inayoshughulikia pamoja na yale ya jamii nzima ya binadamu popote walipo. Fasihi isaidie tabaka la wanaodhuria wanyonge katika jamii yeyote kupambana na matatizo yao yanayo wakabili.
G. Kazilahabi ameonesha kuwa fasihi halisiina msingi yake katika jamii. Baadhi ya viini vya fasihi halisi ni:-
- Kuielewa jamii na mazingira yake(ya kijiografia na utamaduni).
-Kuelewa matatizo ya jamii hiyo.
-Kuelewa ngazi za kijamii na tofauti za kiuchumi(matabaka).
-Kutoa makosa na kuashambulia watu wa ngazi zote bila huruma.
-Kuitazama kwa uangalifu Serikali ya utawala.
Hivyo ili fasihi yetu iwe na manufaa ni muhimu waandishi waandike juu ya matatizo waliyo na hakika nayo wasishughulikie matatizo yalyo nje ya jamii yetu na mwandishi anayeandika matatizo ambayo yako nje ya jamii yetu atakua anaandika nje ya jamii yake.

FASIHI KAMA CHOMBO CHA UKOMBOZI
Ukombozi ni harakati za jamii yoyote zenye lengo la kuitoa jamii hiyo kwa nguvu (kwa silaha) au kwa mazungumzo kutoka katika makuchaa ya watumwa kisiasa,kiuchumi,kimawazo na kiutamaduni.Jamii inaweza kuwa ni ya kitumwa kisiasa ikiwa haitakuwa na fursa ya kushika hatamu ya uongozi wao na badala yake ikategemea uongozi kutoka kwa jamii nyingine jamii itaitwa ya kitumwa ,kiuchumi,ikiwa haitakuwa na haki ya kuendesha njia mbalimbali za uzalishaji mali.Pia jamii isiyoweza kufikiri na kuamua wala kutokuthamini mawazo yake yenyewe na badala yake ikawa katika mgawanyiko wa ibada na itikadi za kigeni ni jamii isiyo huru kimawazo vile vile jamii haitakuwa huru kiutamaduni ikiwa itakosa kuthamini aminifu,uumbaji na ugunduzi wake yenyewe badala yake ikasujudu amali zilizo na chimbuko kutoka nje.
Nyanja za ukombozi wa jinsi fasihi ya Kiswahili ilivyozitazama mpaka leo
(a)Kisiasa
Ukombozi wa kisiasa unapatikanaje?
Unapatikana tu baada ya kupiania uhuru wa bendera kuwa ndio wa kwanza kupatikana kwa nchi ambayo iko katika harakati za kujikomboa katika maandishi ya mengi fasihi ukweli huu unajitokeza kwa mfano katika utenzi wa uhuru wa kwenya msanii anatuonyesha  juu ya vita vya kumngoa mkoloni kutoka katika kiti cha uongozi kwanza baada ya mwafrika kupandisha bendera yake mambo mengine yafuatevilevile katika utenzi wa uhuru wa Tanganyika na utenzi wa jamhuri ya Tanzania “tunaona uhuru wa bendera ukielezwa kwa kabla ya ukombozi wa aina nyingine kufuata.
Kwa hiyo ukombozi huu mwanzo (uhuru wa bendera) husababisha uhuru wa kisiasa wan chi kisha uhuru wa kisiasa huwa ni jukwaa la ukombozi wa uchumi na mambo mengine,vitabu vingine vinavyozungumzia ukombozi wa kisiasa ni mzalendo,F.E.MK Senkero) Ubeberu Utashindwa(J.K Kiimbila),Tone la Mwisho(E.Mbogo),Kinjikitile na Mashetani(E.Hussein),Nuru mpya(R.Rufeshobya)
(b)Kiuchumi
Uhuru wa bendera ni sehemu ya mwanzo tu wa ukombozi wa jamii nchi zinaweza kujidai ni huru kumbe uchumi wake bado ungali mikononi mwa nchi nyingine.Nchi nyingi zinazoendelea bado ziko katika harakati hii ya kutaka kujikomboa kiuchumi.
Waandishi wengi wa fasihi ya Kiswahili  wamezungumzia sana suala la uchumi katika (Mashairi ya Azimio la Arusha) mwandishi anaonyesha na kushambulia unyonyaji ambao ni adui wa uhuru wetu.
Vilevile waandishi wanasisitiza kufanya kazi kama njia ya kuimaisha uchumi.Pia wameeleza kuwa unyonyaji unaweza kukomeshwa kwa kutaifisha njia zote za uzalishaji mali na kuwa mikononi mwa umma.
Katika tamthiliya ya “Bwana Mkubwa” (J.P Mbonde) ameonesha kuwa shabaha yetu sisi ni kupigana na ukoloni mambo leo.Kwa sasa na kupata uhuru kamili.Ukoloni mambo leo ni kikwazo cha ukombozi wa kiuchumi
Kwa sababu ya ulegevu wa uhuru wa kisiasa tunaweza kuwa na mali mikononi mwetu lakini tukizembea kufanya kweli ipasavyo yaweza kufanyiwa njama na ukoloni ndio maana upo umuhimu wa bidii katika kazi na uzalishaji wa mali kisha linafuata swala la ulinzi wa mali hiyo.
Kuzikomboa njia za uzalishaji mali hakutoshi kwani kila hila zao zisizoisha wakoloni wanaweza wakatupora mali hiyo tunapaswa kuwa macho.
Katika utenzi wa “Zindiko la ujamaa” mwandishianaeleza utaifishaji wa njia kuu za uchumi na uhalali wa utaifishaji huo. Mwandishi anaonyesha kuwa utaifishaji huo ulifanywa si kwa kuwaona wakoloni kwa dhuluma bali kama njia moja wapo ambayo itaongeza kwenye ukombozi wa kiuchumi katika jamii. Lengo moja ni kufuata ubinafsi ambao unarutubisha tofauti za kitabaka na badala yake manufaa ya umma kwa ujumla yapatikanayo;
Ukombozi wa kiuchumi si utaifishaji wa njia za uzalishaji mali tu na wala si kukomesha ukabaila na ubepari bali ni kuongeza juhudi katika kazi mbali mbali ili kuongeza kiasi cha pato la kitaifa. Waandishi wengine wanazungumzia ukombozi wa kiuchumi ni kama vile, “Nuru mpya” (G. R. Ruteshubya) “Mashetani” (E. Hussein) “Sauti ya dhiki” (A. Abdallah) “Kasri ya mwinyi fuad” (Shafi Adam Shoji) Zetu bora mkulima na wasifu wa sili binti saad(S. Robert).
C) Kimawazo
Ukombozi wa kimawazo ni uhuru wa mtu katika upeo wa fikra pasipo kutegemea mtu mwingine. Hapa mtu aliye huru awe anajiamini mwenyewe na awe mtu kama watu wengine. Awe mwenye uwezo wa kuwaza, kuamua na kutenda, kuchanganua na kupanga kama watu wengine. Mtu aliye mtumwa na kimawazo anaweza kufananishwa na mnyama wa kufugwa. Mnyama wa kufugwa daima ni masaibu na bwana wake wakati wote huongojea amri kutoka kwa bwana wake.
Maandishi ya fasihi yanazungumziakwa upana swala hili la uhuru wa mawazo . Katika riwaya ya “Njozi za usiku” dhana hii ya utumwa wa kimawazoipo ndani ya watu wengi ambao wanashiria hasa baada ya maajilio ya elimu iliyokuja pamoja na ukoloni na ikatumika kwa upotofu. Katika riwaya hii msanii anaonyesha kuwa wale waliosoma walidharau kazi zote za mikono, walifikiri kuwa kazi za mikono, walfikiri kuwa kazi za mikono michafu na zinafaa kwa wale ambao hawakusoma. Wao wanfikiri kuwa kazi ya mtu aliyesoma ni kushika kalamu na kuandika tu au kuwasimamia ambao hawakusoma.
Tangu uhuru wa Tanzania kumekuwa na harakati za kufutilia mbal ukanganyifu wa namna hii katika mawazo ya watu. Mawazo ya namna hii ndio yamekuwa yakiwafanya watu wengi wa hali ya chini waamini kuwa uchumi walionao wamepewa na Mungu.
Vile vile kimawazo watu waliamini kwamba kila jambo lilitokana na watawala wa kizungu lilikuwa ni bora kabisa. Kwa mfano hata majina yliletwa toka Ulaya  nay a kwetu ya asili kuachwa. Haya yanajadiliwa wazi katika tamthiliya ya “Bwana mkubwa” (J. P. Mbonde)
Katika ukombozi wa kimawazo kuna swala la ukombozi wa mwanamke na swala la dini.
Katik swala la ukombozi wa mwanamke watu wengi wanalitazama krahisi jambo hili. Wengi wanadhani kuwa mwanamke hana haki ya kujibagua kutoka kwa wanaume na kujipigania haki yake. Watu hawa hawaelewi ni mapinduzi gani ambayo hawa wanapigania.
Katika fasihi ya Kiswahili Shaban Robert amepata kuwatetea wanawake katika kazi zake mbali mbali ikiemo Diwani ya”Wasifu wa siti binti saad” na siku ya watenzi wote.
Shaban Robert amemtazama mwanamke kama mtu asiyestahili dhima na utu kama watu wengine wowote wale.
Katika kitabu cha “Wasifu wa Siti binti Saad” msanii au mwandishi anaeleza wazi jinsi jamii ilivyomfanya mwanamke kama chombo cha kutunzwa utawani ili kiwe kizuri kipate kuwavutia wanaokitafuta na baada ya kutoka utawani kikawa mikononi mwa mwanaume kikamtegemea kwa hiyo mwanamke alikuwa ni mtu aliyechukuliwa kama hana wajibu wowote wa maana Zaidi ya kuwa mtegemeaji. Lakini Shabn Robert aliona kuwa ( uk 23) “Ukimdumisha mtu leo utamuona juu ya kilele cha utukufu kesho. Dhila au dhana ililipua fataki ya utukufu katika moyo na mtu mara kwa mara.
Mawazo ya mwandishi ni kwamba wanawake budi watazamwe katika hali zao za maisha katika ubaya na uzuri kama wanaume. Kuhusu swala la dini linajitokeza katika riwaya ya “Kichwa maji” ambapo mwandishi anaona dini imeanzishwa na waoga ambao hutawaliwa na milango yao ya fahamu badalaya kutawaliwa na akili au bongo zao.
Jambo muhimu katika kumkomboa mtu kimawazo ni kwamba ikiwa dini itaendelea kuwepo isiwe na mtazamo duni na finyu na thari zake ambazo alikuja nazo mkoloni akidai kuwa tamaduni zetu ni za kishenzi. Sharti elimundiyo iwe ya kutafakari na kugeuz mfumo wa maisha ya jamii.
Katika dini pia kuna madhehebu mbali mbali ambayo kati yao kuna uhasama mkubwa, mwislamu anadai kuwa yeye ni bora Zaidi kuliko mkristo na mkristo anajiona yeye ni bora kuliko mwislamu. Madhehebu yote haya yamechimbuka huko mashariki ya kati…….katika kitabu cha “Bwana mkubwa” (uk 18-19)
…………kwanini basi mlitutengnisha katika vikundi vidogo vya madhehebu tofauti kada ya wakristo iwapo Mungu ni yule yule mmoja leo mnatueleza tuombe kuungana, utengano alianzisha nani? na kwa faida ya nani?........mbona babu zetu walimwabudu Mungu wao toka zamani kabla ya ujio wa wazungu.
Kwa ujumla dini imechangia kwa kiasi kikubwa sana katika kudumisha mtu kimawazo na kumfanya atumie fahamu tu kwa hiyo katika kumkomboa mtu kimawazo sharti suala la dini litupiwe jich kali fasihi inazidi kuona jicho lake.

(d)Kiutamaduni.
Kwa ujumla utamaduni wan chi zilizotawaliwa na ukoloni umeathiriwa sana na ukoloni huo watu wa nchi hizo wanazipoteza kidogo kidogo thamani za utamaduni zao.
Katika fasihi ya Kiswahili ukweli huu wa mambo tunaupata katika kitabu cha “Njozi za Usiku” mwandishi wa riwaya hii ameelezea namna vijana wote hasa waliosoma hawataki kabisa kusikza kuhusu mila na desturi na michezo ya wakale wao (uk 51)
Hadi leo vijana wengi wakiwa kwao (vijijini) na ikatokea kwamba kuna ngoma za kienyeji zinachezwa wao husimama mbali au kando wakitazama kwa dharau mambo yanayotendeka mbele yao.Wanaamini kabisa kuwa ngoma hizo ni za kishezi ngoma ambazo zinafaa kuchezwa na watu wasiosoma watu wasio staarabika.
Katika riwaya ya “Kichwa maji” mwandishi ameonesha jinsi isiyo ya kawaida kwa msomi au watu wenye cheo serikalini kucheza ngoma za kienyeji lakini vijana hao hao mwanzoni wasomi wenye mwawzo ya kisiasa wakisikia sehemu fulani kuna mziki au disko watajitahidi sana ili wasikose kufika huko.
Kwa sasa kuna mtindo mwingine wa kupaka madawa ya kujichubua ngozi waonekane weupe na wengine huvaa nywele za bandia au maiti ili kuficha nywele zao za kipilipili.Huu wote ni utumwa wa kimawazo kwa upande fulani watu hawa wanaamini kuwa uzungu ndilo shina za maarifa watu hawa hawajui kwamba kuna wazungu wengine ni maskini zaidi hata kuliko sisi wenyewe.
Hitimisho lugha ya ukoloni mambo leo vile vile ili tujikomboe katika nyanjo hizi ni lazima tuondoe ubinafsi, uroho wa madaraka na ulevi wa madaraka hapa nchini.

FASIHI NI SANAA.
Sanaa ni uzuri unajitokeza katika umbo zilizosanifwa umbo ambalo mtu hulitumia kuelezea hisia zinazomgusa kwa kutoa kielelezo au vielelezo vyenye dhana maalumu.
Kazi za fasihi zipo katika nyanja zifuatazo uchoraji, ususi, fasihi, ufinyanzi, muziki, ufumaji, utarizi na maonesho.Nyanja hizi za Sanaa zinaweza kuonyeshwa kwenye kielelezo hiki:-
Ufumaji
Muziki
Utarizi
                                          
Uchoraji
 


     SANAA
        Fasihi
                                                                                    
Ufinyanzi
FASIHI                                  SANAA
                                                                                            
        Uchongaji
Maonyesho
Ususi
 







Katika kipengele cha Sanaa kinachotofautiana na kipengele kwa umbo na matumizi. Fasihi ni kipengele cha Sanaa kinachotumia maneno kuumba huo uzuri wa kisanaa.
TOFAUTI KATI YA FASIHI NA TANZU NYINGINE ZA SANAA
1.       Lugha , kazi zote za kifasihi zinaundwa kisanaa kwa kutumia lugha inayotumika au kuandikika. Lugha hiyo hubeba maana Fulani (ujumbe) kwa jamii Fulani.Hivyo lugha ndiyo inayotufautisha fasihi na Sanaa nyingine. Kwa mfano, uchoraji kipengele chake muhimu kalamu, rangi na kipande cha nguo au karatasi. Ufinyanzi lugha yake ni udongo , uchongaji wa vinyago lugha yake ni gogo la mti n.k
Fasihi si maeezo ya kawaida kawaidakama vile matangazo, taarifa ya habari au barua, fasihi ni maelezo yenye mguso kisanaa. Kazi za kifasihi, huumbwa kimafumbo hutumia nahau au misemo , methali, tamathali za semi, taswira na ishara mbali mbali. Kazi za fasihihufikirisha mtu huweza kutumia akili ili aweze kugundua kazi ya kifasihi aliyosoma au kuisikia kuwa ina maana gani.
2.       Wahusika,kazi yoyote ya fasihi inakuwa na wahusika wake ambao matukio mbali mbali yanayohusu jamii huwazungukia wahusika ni watu ama viumbe, waliokusudiwa wawakilishe tabia za watu katika kazi za fasihi. Kwa upande mwingine wahusika ni muhimu sana katikakutoa na kufikisha dhamira kwa hadira iliyokusudiwa na mwandishi.
3.       Mandhari, kazi ya fasihi inakuwa na mandhri ambayo huonyesha tukio linaponyika. Mandharihiyo inaweza kuwa ya kubuni au ya kweli.
4.       Utendaji, utendaji hasa katika fasihi simulizi hushirikisha fanani na hadhira kwa wakati mmoja. Vile vile utendaji humfanya fanani aweze kuonyesha baadhi yamatendo katika usimulizi wake.
5.       Fani na maudhui,kazi za fasihi zina sehemu mbili yaani fan na maudhui na sehemu hizi zinafungamana. Maudhui ni kile kinachosemwa na fani ni namna kinavyosemwa. Kazi nyingine za Sanaa vile vile zinafanikisha ujumbe kwa hadhira lakinimbinu na vifaa vinavyotumika ni sehemu ya fasihi. Kwa ujumla kazi za kifasihi, fani na maudhui yake ni hali ya juu sana ukilinganisha  na Sanaa nyinginezo.
KWA VIPI FASIHI NI SANAA ?
Usanaa wa fasihi hujitokeza katikavipengele mbali mbali kama ifuatavyo:-
1.       Mtindo, Sanaa kaitka fasihi hujidhihirisha katika namna kueleza jamii (mtindo) katika kueleza jambo kunakuwa na aina fulani ya kiufundi ambao mwanafasihi huutumia katika kufikisha ujumbe kwa jamii yake. Taarifa ianyotolewa inaweza kufichwa katika fumbo, shairi, kitendawili, tamthiliya au hadithi.
2.       Muundo (mpangilio maalumu wa matukio) katika kazi ya fasihi, matukio yanapangwa kiufundi ili yaweze kuwasilishwa vizuri kwa jamii husika. Matukio hayapangwi ovyo ovyo tu bali yanakuwa na mpangilio maalumu.
3.       Utenzi mzuri wa lugha iliyojaa nahau, misemo, methali, tamathali za semi, taswira na ishara mbali mbali unaonyesha wazi usanaa wa fasihi. Lugha itumikayo katika fasihi ni ya kisanaa. Ni lugha iliyopambwana inayokusudiwa kuibua hisia za namna Fulani ka hadhira yake. Lugha hiyo inaweza kuchekesha, kukejeli, kubeza, kuchokoza, kutia hamasa au kushawishi. Matumizi ya lugha yak ya aina tofauti, kuna tamathali za semi, misemo, nahau, methali. Lugha ya wahusika hasa lahaja zao, uchaguzi wa msamiati, miundo ya sentensi, ufundi wa kutoa maelezo hasa ya wahusika ya mandhari na matukio, uteuzi wa lugha yenyewe itumiwayo.
4.       Uundaji wa wahusika, wahusika huwa na tabia zinazotofautiana kati yao.  Wanaundwa kiufundi sana na msanii anaweza kuamua anataka wahusika wanaowakilisha tabia na matendo fulani tu katika jamii na kwa hiyo atawaumba wahusika hao ili kukamilisha nia na lengo lake.
Katika kutofautisha tabia na hali za wahusika, mwandishi analazimika kutumia mbinu ya kuwapa majina wahusika wake. Wahusika wanaweza kuumbwa kinafsi au kiakili na kimwili. Kutokana na ujenzi wa aina hii mhusika huonyesha wasifu wake wa ndani na nje au anaweza kuonyesha mabadiliko yake kila anapokutana na mazingira tofauti.
5.       Mandhari, fasihi hujengwa katika mazingira maalum. Mandhari husaidia sana kujenga hisia inayokusudiwa na mwandishi. Mandhari yanajengwakiufundi na mwandishi ili yasaidie katika kujenga kazi nzima ya fasihi.

MASUALA YA KIITIKADI NA DHANA YA UDHAMINI KATIKA KAZI ZA FASIHI
Maana ya Itikadi
Itikadi ni Imani ya watu au jamii Fulani juu ya kitu Fulani. Itikadi kisiasa ni mfumo wa mawazo na Imani ambao umewekwa na tabaka tawala/ tawaliwa au tabaka lolote lenye nguvu katika jamii inayohusika ikiwa na lengo la kulinda, kutetea na kuendekeza matakwa na maslahi yake. Utaratibu huo unaambatana na umilikaji wa njia kuu za uchumi na umilikaji wa mapato ya ziada yatokanayo na jasho la wazalishaji mali hizo, vymbo vya kitaalumakama vile elimu na nyenzo zisaidiazo kuimarisha itikadi kama vile dini vinatumika kutetea utaratibu uliowekwa na tabaka tawala.
Kimsingi kuna mitazamo miwili ya kiitikadi:-
i)                    Itikadi inayotetea na kulinda maslahi ya watu wchache tu katika jamii (utumwa, ukabaila na ubepari)
ii)                   Itikadi inayotetea na kulinda maslahi na matakwa ya watu wengi katika jamii (ujima na ukomunisti).
Vile vile tunapojadili juu ya itikadi katika fasihi na usemi kwa ujumla pia tunaongelea juu ya utabaka uliopo katika jamii inayohusika . Kuna matabaka ya aina mbili:-
a)      Tabaka tawala
b)      Tabaka tawaliwa
Tabaka linamiliki vyombo vya dolana kwa kutumia vyombo hivyo na kwa kutumia waandishi, tabaka tawala linaunda, linaendeleza na kutetea maslahi yake.
Vile vile tabaka tawala lina nguvu za kiakili na za kielimu kwa manufaa yao. Mwandishi kwa ujumla hawezi kuepukana na mfumo huo wa kitabaka. Tabaka Fulani huwa dhamini waandishi kwa njia mbali mbali.
UDHAMINI
Ni hali ya watu au shirika Fulani kutoa fedha kwa ajili ya kugharimu kitu fulani . Mdhamini au wadhamini ni kundi la watu wenye shabaha zinazofanana wenye kusimama kama ufadhili wa mradi fulani. Katika fasihi hawa ni wale wanaosimamia makundi maalumu kipropaganda na kiitikadi.
AINA ZA UDHAMINI
Kuna udhamini wa aina mbili:-
i)                    Udhamini wa ushawishi
ii)                   Udamini wa nguvu

UDHAMINI WA USHAWISHI
Ni aina ya udhamini ambao mdhamini huwashawishi na kwanunuawaandishi au wasanii. Matokeo yake ni kwamba msanii anafungwa na matakwa ya mdhamini.
UDHAMINI WA NGUVU
Huu ni udhamini unaotumia vyombo vya dola kama vile jeshi, polisi, magereza n.k.Hakuna hiari katika udhamini wa nguvu, kila kitu kinaendeshwa kama vile mashine tu. Kwa ujumla mwandishi akidhaminiwa kwa nguvu za serikali huwa kama kasuku aimbaye na kuutukuza mfumo wa maisha uliopo katika jamii hata kama roho na moyo wake viko mbali sana na mfumo huo. Lakini msanii anapodhaminiwa kutetea umma, lazima kutakuwa na madhara yake katika jamii yake inayohusika.
Mwandishi wa fasihi katika kila nchi atakuwa na udhamini unaolingana na mazingira yake kwa mfano katika nchi ya Tanzania, mwandishi anaweza kuandika kwa udhamini wa jamii yake inayohusika.Mdhamini anaweza kuwamtu binafsi mwenye fedha, shirika, chombo cha serikali, chama Fulani au kundi la mataifa kwa ushirikiano. Pia mdhamini ni mwakilishi wa wenye mamlaka juu yake, kwa mfano katika serikali yaTanzania chuo kikuu ni mwakilishi wa serikali na serikali ni mwakilishi wa tabaka tawala. Hivyo msanii anayedhaminiwa na chuo kikuu ambacho ni combo cha serikali hatimaye anajikuta anafanya kazi ili kuendeleza maslahi ya tabaka tawala.
SABABU ZA UDHAMINI
Ø  Uhaba wa fedha kwa waandishi za kuendeshea shughuli zao za uandishi katika uandishi wa kazi za fasihi. Pesa zinahitajika kwa ajili ya kununulia karatasi, kalamu, uchapaji n.k.
Ø  Kulinda na kutetea maslahi yawadhamini wao. Hii inatokea zaidi kama mdhamini ni wa tabaka tawala. Kama tabaka linalo tawala ni la mabepari kazi za fasihi zitatetea tabaka hilo.
Ø  Kujulikana au kuipendekeza. Baadhi ya waandishi hudhaminiwa kwasababu ya kutakakujulikaa na kwa upande mwingine mdhamini anawadhamini waandishi kwa lengo hilo.
Ø  Kupata fedha za haraka. Hawa huandika vitabu vyenye kujaa wahusika wakuu, mafundi wa kufanya mahaba, kutumia madawa ya kulevya na kufanya mapenzi kwa kutumia mipira ya kiume na kike bila kujali stahana utamaduni wa jamii yake. Mwandishi anachojali hapa ni pesa na sio matakwa ya jamii yake.
Ø  Kulazimishwa na tabaka tawala. Waandishi hawawanakubali udhamini huo kwakuogopa udhabiti wa kazi zao na tabaka tawala. Waandishi hawa wakikataa udhamini huo kazi zao zitadhibitiwana kupigwa marufuku zisisomwe au kuchapishwakabisa.

ATHARI ZA UDHAMINI
1.       Mwandishi anayedhaminiwa anatakiwa kuandika yale tu ambayo mdhamini wake anayataka. Msanii hatakuwa na hiari au uhuru wa kuandika kitu chochote na kwa njia anayotaka. Kwa kudhaminiwana tabaka tawala kamwe mwandishi hawezi kudharau umma ili ujitambue kuwa unagandamizwa.
2.       Mapana ya uandishi wake kidata, kigiografia na kimaudhui huamuliwa na mdhamini na kutegemea mahitaji yake na kiwango cha fedha alichonacho mdhamini.
3.       Ufafanuzi wa data na maudhui ya kazi ya fasihi lazima ulingane na mtazamo wa itikadi ya mdhamini.Hii ina maana kuwa mwandishi wa kazi ya fasihi hawezi kufanya ufafanuzi wa data na maudhui mwenyewe bila kumshirikisha mdhamini.
4.       Matokeo ya uandishi wa kazi za fasihi mara nyingi ni mali ya mdhamini na hutumia kuendeleza maslahi yake mabayo sio lazima yalingane na malengo ya mwandishi.
5.       Wasanii au waandishi wengi kutokana na kudhaminiwa huanza kuandika kazi zao kwa kupenda pesa hii huwafanya waandishi kuwa makasuku kwa sababu ya kuandika yale tu yasemwayo na mdhamini wake bila kuyafanyia uchambuzi wa kina.
6.       Udhamini hukuza utabaka katika jamii, hapa tunakuwa na tabaka lenye nacho (mdhamini) na tabaka la wasionacho (msanii) mdhamini humnyonya msanii.
7.       Kuzuka kwa fasihi pendwa (riwaya ya pendwa).Hapa waandishi kwa lengo la kupata pesa za haraka huandika riwaya pendwa ambazo zina soko kubwa hapa nchini hasa kwa vijana na wakati huo huo riwaya hizo hazifunzi lolote jamii Zaidi ya kuburudisha.
8.       Udhamini huchochea rushwa, hii ni kwa sababu waandishi wengi wanataka udhamini huo na matokeo yake wale wanapata udhamini huo lazima watoe chochote (rushwa) kwa mdhamini.


UMUHIMU WA UDHAMINI
1.       Husaidia waandishi chipukizi katika kuchapisha kazi zao.
2.       Husaidia waandishi katika kufanya utafiti wa mambo mbalimbali yatakiwayo katika Sanaa hiyo ya fasihi.
3.       Husaidia kufikisha ujumbe kwa hadhira kwa kukuza taaluma ya uandishi.
UHURU WA MWANDISHI
Dhana ya uhuru wa mwandishi ni pana sana.
Kwanza uhuru wa mwandishi uko katika utashi,Bila utashi mwandishi atakuwa mwoga na mwepesi wa kukata tamaa.Atayumbishwa haraka kutoka kwenye msingi wa falsafa yake na Imani aliyo nayo juu ya mabadiliko yatokeayo katika jamii.Makombora ya wahakiki na wanasiasa huweza kumyumbisha, lakini kwa mwandishi mwenye utashi makombora hayo humkomaza.
Baadhi ya waandishi walionyesha utashi wao katika Afrika ni Ole Sanyika na Ngugi wa Thiongo “waandishi hawa wameshambuliwa sana na wahakiki, lakini misimamo yao ni ile ile vile vile wamewahi kufungwa na walipotoka kifungoni hawakubadili misimamo yao na wamekuwa hivyo kwa sababu ya utashi wa falsafa zao katika fasihi ya kiswahili, waandishi wenye utashi wapo na msini wa kuwepo kwao ni kutoyumbishwa na matamshi ya jukwaani na wahakiki ambao hawajapevuka.

Pili,uhuru wa mwandishi umo katika kuwa na falsafa moja inayoeleweka,Falsafa ifanyayo na maandishi ya mwandishi moja yawe na kitu kijulikanacho lengo.Waandishi waliotajwa hapo juu yaani Ole Sanyika na Ngugi wa Thiongo ndio wanaongoza kuwa na falsafa zao zinazojulikana. Katika fasihi ya Kiswahili tunaona waandishi wachache wenye falsafa zao inayojulikana wengi tulio nao wanaandika kufuatana na jambo fulani au tukio la wakati huo bila kulinganisha leo ataandika juu ya mapenzi, kesho juu ya upelelezi na kesho kutwa mapinduzi mwishowe anakuwa na orodha ndefu ya vitabu visivyokuwa na lengo.
Waandishi wachache tulio nao ambao wameelekea kuwa na falsafa inayoongza maandishi yao ni kama Shaban Robert, G.Kezilahabi na Mohamedi Suleiman.Bila kuwa na falsafa maalumu ni rahisi kwa mwa mwandishi kuyumbishwa.
Tatu, uhuru wa mwandishi umo katika kuitawala vema Sanaa yake,kama unaandika riwaya na hujui misingi ya Sanaa ya aina hiyo atajikuta katika kikwazo,utajikuta uhuru wa kisanaa unaweza kujaribu, lakini kazi utakayoitoa itakuwa hafifu.Kazi nzuri ya kisanaa ni ile inayounganisha vema ubunifu na uhalisia.Mwandishi akielemea sana katika ubunifu anazua matatizo mengine kazi ngumu aliyonayo mwandishi ni katika kupata barabara msitari huo.Mwandishi mwenye vitabu vingi anaweza kuwa na kitabu kimoja tu kilichoupatia vema mstari huo katika fasihi ya Kiswahili waandishi walioupatia msitari huo tunao.Ebraim Hussein,Penina Mhando,Mohamed Suleiman, C.G Mng’ong’o na J.A.Safari.Msanii anayeweza kuitawala  vema Sanaa yake anaunganisha vizuri Sanaa na maudhui yake.
Mwisho uhuru wa mwandishi umo katika lugha anayotumia msanii atawale vema Sanaa yake nilazima ujue lugha anayotumia.Lugha ndicho kiungo maalumukati ya Sanaa na kazi ya kifasihimwandishi kama hajui vema lugha anayotumia atajikuta hana uhuru wa kukisema anachotaka kwa hiyo lugha ndiyo nguzo ya nne katika uhuru wa mwandishi, waandishi wa Kiswahili  waliokwisha kutajwa wanakitawala Kiswahili sanifu,Kiswahili sanifu ndiyo msingi
wa fasihi ya Kiswahili.
Ni kweli kuna uhuru wa mwandishi?
Uhuru wa mwandishi ni nini?
Ni ile hali ya mwandishi wa fasihi kuwa huru na wazi katika kutoa mawazo au hisia zake kwa jamii.Ni uhuru wa kuandika na kulikosoa tabaka lolote katika jamii bila kupata matatizo yoyote.
Mwandisihi ni nani?
Ni mtu yoyote atumiaye muda wake mwingi  kuandika na kuzungumzia jamii yake kwa njia ya maandishi.
Je kuna uhuru wa mwandishi?
Kwa ujumla uhuru wa mwandishi ni uhuru ikiwa hakufaulu kudhuru tabaka tawala hii ni kwa sababu suala la uhuru wa mwandishi ni la kitabaka na lilianza pale jamii ilipogawanyika katika matabaka kwa maana hii uhuru wa mwandishi unaamuliwa na tabaka tawala
Kuanzia enzi za utumwa, maandishi ya liyovumbuliwa fasihi andishi ya mwanzo ilikuwa ya wateule wachache tu na wenye vyeo vyao.Hao mabwana, wamwinyi na mabepari walihakikisha kila mbinu hutumika ikiwemo ya udhibiki wa maandishi kuendeleza na kulinda utawala wao.
Naye B.Goya (1974-78) anasema kwa maandishi hana uhuru kwa vyovyote vile kwa sababu yeye ni tokeo la jamii Fulani kila jamii ina mipaka yake ambayo mtu hatakiwi kukiuka kwa vyovyote vile mwandishi huyu amebanwa na mipaka hiyo asivuke.Pindi avukapo mipaka hiyo atapambana na jamii hiyo (tabaka tawala) vitabu vya mwandishi huyo vitapigwa marufuku au vitabu vikitolewa havitanunuliwa au serikali itavikusanya na kuvifanyia mipango mwingine katika Afrika  kuna mifano mingi ya udhibiki wa waandishi mfano mzuri ni mwandishi maarufu wa Kenya Ngugi wa Thiongo ambaye kazi zake hasa ya “Ngaahika Ndeenda”(I will marry when I want)- Nitaolewa Nitakapotaka, Ilimgombanisha na vyombo vya dola hadi akawekwa kizuizini, Ngugi wa kwanza kufichua siri za mfumo wa kibepari kwa watu wanyonge aliliuzi tabaka tawala la jamii yake ambalo halikusita kutumia udhibiki na vyombo vyake vya Mabavu.

Baada ya uhuru vitabu vingi sana viliandikwa kwa kudhibitisha maandishi mbalimbali uliojitokeza waziwazi E.Kazilabi aliandika riwaya “Rosa mistika”(1971) kitabu hiki kilipigwa marufuku kisitumike mashuleni na wala kisiuzwe waziwazi madukani.Ilidaiwa kuwa waliokipiga marufuku kuwa kilikiuka maadili ya jamii kwa kueleza mambo ya aibu kwa wazi.Sura ya kumi ndiyo hasa ilitolewa mfano wa uchafu wa kitabu hiki.Udhibiti huo ulifanywa na Wizara ya Elimu na ulizusha maswali mengi kwa wasomaji.Wasomaji walianza kujiuliza, Je si kweli uchafu uelezwao katika “Rosa mistika” umo ndani ya jamii ya Tanzania? Je upotofu na uongozi mbaya ulifuchuliwa na riwaya hiyo hii si upo kati yetu? Kwa baadhi ya wasomaji ilielekea kuwa suala la uchafu wa maelezo yatokeayo kitandani baina ya wakuu wa chuo na wanafunzi wake lilitumika kama kisingizio tu cha kudhibiti ukweli wa masuala mengine nyeti yaliyowagusa viongozi wakilishwa na watu kama vile Bwana Maendeleo Deogratius anayeshiriki katika kuwaharibu vijana.
Vitabu vingine ambavyo havieleweki vinasema nini, maudhui, falsafa na ujumbe wa mwandishi ni mashetani(E.Hussein) “Aliyeonja Pepo”(F.Topan) na “Ayubu” Paukwa theatre Association.Na hivi viko kwa kukwepa mkono mrefu wa tabaka tawala.

DHIMA YA UHURU WA MWANDISHI.
1.       Mwandisshi atakuwa huru kuikosoa jamii au tabaka lolote litakaloenda kinyume na utaratibu wa jamii bila matatizo.Mwandishi atakuwa huru kuonyesha dhuluma, ukatili na ujangili unaofanywa katika jamii na tabaka lolote bila matatizo yoyote.
2.       Kukiwa na uhuru wa mwandishi, msanii atakuwa na falsafa inayoeleweka pamoja na utashi (wake).Hii itamfanya mwandishi awe na msimamo unaoeleweka.Msimamo  wake utamaidia kuifundisha na kuielimisha jamii bila uoga.Ataijiulisha jamii hali yake na ataonesha jamii njia za kufikia haja na kutatua matatizo ya jamii bila uoga
3.       Mwandishi atakuwa huru kutoa mwongozo katika jamii kwa kuikomboa jamii kutoka katika fikra mbovu za kugandamizwa, kunyonywa na kuonewa na tabaka tawala ili jamii ipate haki na heshima bila woga wa kuliondoa tabaka ambalo ndilo lenye mamlaka yote katika jamii.
4.       Uandishi wa kikasuku hupungua, waandishi au wasanii huacha tabia ya kuwa vipaza sauti vya tabaka fulani katika jamii, wasanii makasuku huandika mambo bila kufikiri na kurudiarudia  mawazo yaliyokwisha semwa na wanasiasa majukwaani bila fikra mpya kwa hali hii hupotosha jamii.Hivyo kunapokuwa na uhuru wa mwandishi wa kutosha hali hii haiwezi kutokea kwa sababu mwandishi ataandika mambo mbalimbali yanayojitokeza katika jamii na hataweza kujikomba au kujipendekeza kwa tabaka tawala lenye mamlaka yote katika jamii.
5.       Kunapokuwa na uhuru wa mwandishi fasihi inakuwa chombo cha kuikomboa jamii kiuchumi,kisiasa, kiutamaduni na kifikra (kimawazo) katika jamii ya kitabaka fasihi ni mali ya tabaka tawala na hutumia fasihi kutetea na kulinda maslahi yao.Hivyo inapokuwa mali ya jamii nzima inatumiwa na jamii hiyo katika kuwakomboa wanajamii wote.
6.       Kunapokuwa na uhuru wa mwandishi, mwandishi anakuwa huru kuichokoza na kuisukasuka (kuichochea) jamii bila matatizo yeyote. Mwandishi atachokoza jamii ya wakulima na wafanyakazi kufikiri ili waweze kulichunguza tabaka tawala kwa jicho pevu na kutoa hadharani uozo uliopo katika kunyonywa, kupuuzwa,kuonewa, kugandamizwa na kunyanyaswa na tabaka tawala

7.       Mwandishi atakuwa huru kuelimisha na kuishauri jamii katika mambo muhimu yanayojitokea katika jamii bila woga.Mwandishi ataishauri jamii kuhusiana na mambo kama vile afya, elimu na ichague mambo gani yanafaa kuhifadhiwa na yapi hayafai vile vile msanii anakuwa huru kuirekebisha jamii bila woga kwa kuangalia yapi ni mazuri na yapi ni mabovu yanayotendeka katika jamii  
Share:

No comments:

Post a Comment

ONLINE VISITORS


Labels

Blog Archive

Recent Posts